Alhamisi, 5 Septemba 2013

WALIOWAHI KUWA NA NYADHIFA

tutakuwa tukiwaletea wazee wetu waliowahi kushika nyadhifa mabalimbali ndani na nje ya Tanzania.
je, unamfahamu mzee OMARY HUSSEIN SESEME?
 huyu ni mtoto wa pili kati ya watoto sita wa mzee HUSSEIN SESEME kwa upande wa tumbo la BI, TABU BINTI SAALUM, maarufu kamam HEYAHEYA.
mzee huyu alifanikiwa kuwa na watoto nane(8)

1.Seseme, 2.Abdu 3.Mahmud, 4. Feli, 5. Abasi, 6.Shabani, 7.Safia, 8.Salum.
katika harakati zake za maisha,  alikuwa Askari Magereza, mpaka anastaafu alikuwa na cheo kikubwa sana katika jeshi hilo....................................
 fuatilia kuijua historia yake,alikozaliwa,alikosoma na alikuwa na wake wangapi
 

Jumatano, 10 Julai 2013

HAYA NDIO MAENEO AMBAYO YANATUMIKA KUZIKIWA UKOO WA SESEME NA MATAWI YAKE, MIONGONI WALIOZIKWA MAENEO HAYA NI MZEE HUSSEIN SESEME, MZEE ABDALLAH SESEME, MZEE OMARY SESEME HAWA NI NDUGU WATATU.PIA AMEZIKWA MZEE ATHUMANI , MZEE OMARY , MZEE JAFARY , MZEE MWAMADI, MZEE RAMADHANI, BI KIBIBI, BI MWADAWA, BI SHIDA, NA WENGINE WENGI. M.MUNGU WALAZE MAHALA PEMA PEPONI AMIIN

Jumamosi, 22 Juni 2013

NI MIMI NDUGU YENU BW SHABANI ALLY SESEME NAWALETEA MADA HII YA UMUHIMU WA UMOJA NA MSHIKAMANO KATIKA UISLAMU BISMILLAHIR-RAHMANIR-RAHIIM Assalam alaykum!! Utangulizi Kila sifa njema anastahiki kushukuriwa Allah(s.w),Rehma na amani zimuendee kiongozi wa ummah huu Mtume Muhammad(s.a.w) na juu ya aali zake na maswahaba zake wote(r.a Napenda kuchukua fursa hii tukufu ili niweze kuufikisha ujumbe huu kwa waislam juu ya Umuhimu wa kuwa na umoja na mshikamano baina yetu.Suala la umoja na mshikamano baina ya waislamu ni jambo ambalo Allah( s.w) analisisitiza sana katika kitabu chake kitakatifu.Hivyo basi umoja baina ya waislamu ni jambo la LAZIMA.Ukiangalia katika ibada zote alizotuwekea Allah(s.w) zinahimiza suala la kuwa na umoja na mshikamano baina yetu waislamu.Angalia tu katika nguzo za uislamu jinsi Allah alivyoziweka na zinavyohimiza umoja baina yetu ni wazi kuwa suala la umoja na mshkamano ni muhimu sana katika uislamu.Ibada ya Swala, Funga , Zakat, Hijjah n.k, hizi zote zina himiza umoja na mshikamano baina yetu. Katika kusisitiz suala hilo Allah anasema katika sura ya 49:10 “Hakika Waumini ni ndugu, basi patanisheni baina ya ndugu zenu, na mcheni Mwenyezi Mungu ili mrehemewe. “ Katika aya hii tunajifunza kuwa waislamu wote ni nduga, pale linapotokea tatizo basi hapana budi watu wapatane ili tuweze kujenga umoja utakao kuwa madhubuti baina yetu.Lakin leo ni tofauti waislam wao kwa wao ndio hugombana, hitiliana fitna, majungu n.k hii ni kuonyesha leo hakuna umoja na mshikamano uliopo baina yetu. Kaika maubile ya wanaadamu suala la ikhtilafu ni la kawaida.Allah ametuumba tofauti tfauti wapo wanene, wembamba,warefu, wafupi, weupe, weusi , hizi ni tofauti.Kuzuia ikhitilafu hutoweza kwa sababu ndio maumbile ya mwanaadamu,asichotaka Allah ni FARQA. FARQA baina ya waislam in jambo ambalo Allah alikemea na halipendi anachotaka yeye ni umoja (I’TISWAM) na mshikamano baina yetu.Anasema katika Qur-an sura 3:103-105 “Na shikamaneni kwa Kamba ya Mwenyezi Mungu nyote pamoja, wala msifarikiane. Na kumbukeni neema ya Mwenyezi Mungu iliyo juu yenu: vile mlivyo kuwa nyinyi kwa nyinyi maadui naye akaziunganisha nyoyo zenu; kwa neema yake mkawa ndugu. Na mlikuwa ukingoni mwa shimo la Moto, naye akakuokoeni nalo. Namna hivi Mwenyezi Mungu anakubainishieni Ishara zake ili mpate kuongoka”.Anaendela nakusema .”Na uwe kutokana na nyinyi umma unao lingania kheri na unao amrisha mema na unakataza maovu. Na hao ndio walio fanikiwa”.Anaendelea nakusema .”Wala msiwe kama wale walio farikiana na kukhitalifiana baada ya kuwafikia hoja zilizo wazi. Na hao ndio watakao kuwa na adhabu kubwa. “. Hizi ni aya ambazo Allah anasisitiza waislam tuwe na umoja na mshikano na yeye hapendi kufarikiana katika masiala ya dini na ndio maana yeye anatuambia pale tunapo ikhtilafiana katika masuala ya dini tufanye yafuatayo.Qur-qn 4:59 ‘Enyi mlio amini! Mt'iini Mwenyezi Mungu, na mt'iini Mtume na wenye madaraka katika nyinyi. Na mkizozana katika jambo basi lirudisheni kwa Mwenyezi Mungu na Mtume, ikiwa mnamuamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho. Hayo ndiyo bora zaidi na ndiyo yenye mwisho mwema.” Hivi ndivyo Allah anavyo tufundisha tufanye pale tu tunapo ikhtalifiana katika masuala ya dini yetu nayo ni kuirejea QUR-AN na SUNNAH hiyo ndiyo suluhisho litakalopelkea kupatana kwetu.Sasa basi kwa nini mpaka leo waislamu wamefarakana?.Jibu ni kwamba waislamu tumeacha kuifuata QUR-AN na SUNNAH na ndio maana leo tupo kwenye hali hii. Hivyo basi Allah anatutaka tuifuate QUR-AN na SUNNAH kwani ndio vitu viakavyo tuletea umoja wa kweli na mshikamano baina yetu waislamu.Allah katika Qur-an anatuelelea kwamba yeye anawapenda watu walioshikamana katika dini yake.Anasema katika sura ya 61:4 “Kwa hakika Mwenyezi Mungu anawapenda wanao pigana katika Njia yake kwa safu kama jengo lilio kamatana” Allah anaupigia mfano umoja na JENGO jinsi (material) yaliyo tumika kulitengeneza jingo yalivyo shikamana,.Kama hivyo ndivyo mtume (s.w) anasisitiza katika hadithi ifuatayo: Imepokelewa hadithi kutoka kwa Nu’uman bin Bashiir (r.a).Mtume anasema”Waumini ni sawa kama macho yanauma (yana matatizo)mwili mzima unaumwa (una matatizo) kama kichwa chake kinauma basi wmili mzima unauma”(Muslim) Ndugu zangu katika imani hivi bado hujaelewa tu jinsi suala la umoja na umoja na mshikamano lilivyo kuwa muhimu katika uislamu. Mafunzo tunayoyapata kutokana na aya hizi na hadithi hii ya mtume(s.w) 1. Umoja ni jambo la lazima 2. Atakaye vunja umoja amekeuka amri ya Allah 3. Kpendana baina yetu 4. Umoja na mshikmano ndio ngao kwa waislam. Allah anatukataza katika Qur-an kuwa na makundi makundi makundi katika dini yetu kwani kila kikundi kitasifia upande wake na FARQA itatokea.Allah ansema katika sura ya 30:31-33 “ Muwe wenye kutubia kwake, na mcheni Yeye, na shikeni Sala, na wala msiwe katika washirikina”.Anaendelea “. Katika wale ambao kwamba wameigawanya dini yao, na wakawa makundi makundi, kila kikundi kinafurahia kilicho nacho”Anaendelea “ Yakiwapata watu madhara humwomba Mola wao Mlezi nao wametubu kwake. Kisha akiwaonjesha rehema itokayo kwake, mara kikundi miongoni mwao humshirikisha Mola wao Mlezi,” Ili tuwe na umoja na mshikano kama alivyokuwa mtume na maswahaba zake uliopelekea kuwashinda maadui wa zama zao, Allan anasema sura ya 48:29 “Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu. Na walio pamoja naye wana nguvu mbele ya makafiri, na wanahurumiana wao kwa wao. Utawaona wakiinama na kusujudu wakitafuta fadhila na radhi za Mwenyezi Mungu. Alama zao zi katika nyuso zao, kwa athari ya kusujudu. Huu ndio mfano wao katika Taurati. Na mfano wao katika Injili ni kama mmea ulio toa chipukizi lake, kisha ukalitia nguvu, ukawa mnene, ukasimama sawa juu ya ubuwa wake, ukawafurahisha wakulima, ili kuwakasirisha kwa ajili yao makafiri. Mwenyezi Mungu amewaahidi walio amini na wakatenda mema katika wao msamaha na ujira mkubwa.’ ni lazima umoja huo upitie upitie hatua TATU: 1. Tuwe na lengo moja.(9:33, 61:9, 48:28) 2. Kufanyiana wema baina yetu(hadithi ya mtume) 3. Kutofanyiana mabaya · Dhulma · Kusengenyana · Kuchukiana · Kuvunjiana heshma Sababu za kutokuwa na umoja na mshikamano 1. Hatuna lengo moja 2. Ufahamu wetu juu ya dini tofauti 3. Ufahamu wetu juu ya qQur-an ni tafauti 4. Ufahamu wetu juu ya sunnah ni tofauti Hitimisho:Hivyo basi waislamu ni lazima tushkamane na tuwe na umoja wa kweli baina yetu ili tuzishinde kaumu za makafiri

Jumatatu, 11 Februari 2013


BW.ATHUMANI HUSSEIN HUSSEIN SESEME
je, unafahamu kuwa mzee Athumani ndio mtotot wa kwanza kati ya watoto 16 wa mzee seseme makumbitu?
 fuatilia kwa makini historia yake.

Inakubalika kwamba safari yoyote ile haikosi kiongozi wake. Na katika uzawa wa ukoo huu wa Seseme hapana shaka kiongozi wake ni Bw ATHUMANI                Hussein mtoto wa kwanza wa Mzee Hussein Hussein Seseme. Umefikiwa uwamuzi wa kumtambua hivyo mzee Athumani kuwa huyo ndiye kiongozi wa ukoo huo wa          Seseme kutokana na yeye mwenyewe kufanya mambo mengi mazuri katika kusaidia ukoo kuimarika japokuwa mzee Athumani alikuwa mtoto wa tatu kiuzawa  kuzaliwa. Baada ya kuanza kuzaliwa Bi Mwanakheri Omari Seseme, akifuatiwa na Bi Amina Abdallah Seseme ndipo kisha  akazaliwa yeye bado fikra za wengi zilimpa nafasi kubwa ya uongozi Mzee Athumani. Ni mambo mengi mazuri alioyafanya katika ukoo huu ambayo yangefaa kupigiwa mfano lakini tunachelea kuandika hapa kila jambo kwani itakuwa ni hadithi ndefu kama vile alifu lela ulela. Kwa kifupi mzee Athumani alizaliwa mwaka 1922 bila shaka hapo Mtoni kwa Azizi Ally, na alifariki nyumbani kwake Bungoni Ilala Dar es salaam mnamo tarehe 29/9/2008.

 Mzee Athumani walizaliwa wawili tu upande wa mama yake Bi Chausiku Binti Mwenegoha Kawambwa wa Kingugi, katika ukoo wa Dumbalume. Bi Chausiku alikuwa mke wa kwanza kuzaa na mzee Hussein Hussein.   Maisha ya bibi huyo yaliishia Mtoni kwa Azizi Ally   baada ya kwisha kuzaa wanawe wawili hao, mzee Athumani Hussein na dada yake Bi Mwajuma Hussein, Bi Chausiku                            alipofariki miaka ya 19 hivi alizikwa pembezoni mwa msikiti wa kwa Kombo hapo hapo Mtoni. Aliwaacha Mzee Athumani na dada yake Bi Mwajuma wakiwa bado wadogo sana.

ELIMU.
Mzee Athumani Hussein alipata elimu zote mbili ya dini na dunia , hivyo katika elimu ya dini ya Kiislamu imemjengea imani kubwa katika Uislamu hadi kuwa muumini wa kweli wa Kiislamu ambaye akifuata  maagizo yote ya dini itikadi.              Alikuwa Hamsa swalawat asiyependa kupitwa na hata kipindi kimoja cha swala katika umri wake wote hadi alipofariki.


Kwenye miaka ya hamsini hadi sitini alipata kuwa Imamu wa msikiti wa Keko Akida katika kipindi Fulani,, alipokuwa akiishi hapo kati ya mwaka 1952 hadi 1963 mzee Athumani alihamia Keko Akida katika mwka 1952 akitokea Mbagala, kabla ya hapo alipata kuishi mtaa wa Nyamwezi na Kipata eneo la Kariakoo mahala    ambapo mtoto wake wa kwanza Bw. Hassan    Athumani Seseme alipozaliwa kwenye miaka ya 1946 kabla ya kuhama tena na kurudi Mbagala kipindi chote hiki                 alishaanza kufanya kazi Railways  alipoanza kazi Railwaya kunako mwaka 1940 akiwa na umri wa mika 19 hivi.

Akiwa kazini Railways alipata kupelekwa masomoni Nairobi Kenya katika               kuboresha ujuzi wake kama Locomotive Mechanic katika idara ya fittingi shop. Na aliporudi masomoni akapata cheo cha foreman na hatimaye Supervisor. Cheo hiki alidumu nacho hadi pale alipostaafu rasmi mwaka 1977.

Alipohamia Ilala Bukoba Street 31 mwaka 1963 mwishoni aliendelea na Uimamu, hapo alisalisha msikiti wa Pangani na Mwanza mara baada ya kufariki Imamu wa msikiti huo kwenye miaka ya sabini themanini hivi.

Vile vile aliendelea na Uimamu katika msikiti mkuu wa Ilala, Arusha Street kwa muda fulani mwisho alimalizia uimamu katika msikiti wa masjid Taqwa Bungoni wakati huo alikuwa hajiwezi tena kwa kuzidiwa na umri na maradhi ya kiutu uzima.
 Mzee Athumani katika ujana wake wote na hata alipofika kuwa mtu mzima alijishughulisha mno na  mambo ya dini ya Kiislam. Alipenda kujiendeleza kusoma dini na pia alikuwa mwana Twarika mashuhuri sana wa “SHADHIRY”.
Miaka ya 1977 alipostaafu kazi Railways alipata bahati ya kwenda HIJJAH MAKKA.  Kutokana na kujishughulisha sana na mambo ya dini alipostaafu kazi alifanya kazi ya dini BAKWATA, kutokana na uadilifu aliwahi kuchaguliwa na BAKWATA kuwa Sheikh wa Wilaya ya Ilala cheo hicho alidumu nacho hadi kifo chake mnamo mwaka 2008.
Bwana Athumani katika elimu ya dunia alipata kusoma shule ya Mchikichini na hatimaye akaendelea na masomo yake katika shule ya Uhuru Mchanganyiko enzi hizo ikijulikana kama Kitchwele Boys Middle School. Hapa alisoma hadi darasa la nane kisha kujiunga na Railwaays 1940 . Kichwele Boys alipata kusoma na baadhi ya viongozi wa nchi hii Tanzania kama vile mzee Kawawa, Kitwana Kondo na kadhalika . Aliwahi pia kuwa kaka wa shule Prefect hapo Kichwele School.

Inasemekana kuwa elimu yake ya dini alisoma katika madrasa ya maalimu Mzinga eneo la Kariakoo lakini kwa vyovyote vile enzi hizo Masheikh                    waliokuwa wakifundisha walikuwa siyo hawa kina maalim Mzinga                           tunayemfahamu sisi. Kwani kipindi hicho tunachokiongelea ilikuwa miaka ya 1930/1940. Ni yule maalim Mzinga mwenyewe hapo awali aliwahi kusoma             Madrasa  ya baba yake Mzee Makumbitu hapo Mtoni.

Bw. Athumani aliwahi kuoa jumla ya wake wanne wakati wa uhai wake, kila mke kwa wakati wake, hakuwahi kuwa na mke japo wawili tu kwa wakati mmoja.
Mke wa kwanza wa mzee Athumani aliitwa Tuhuma bint Omari alimuoa mwaka 1940. Aliishi naye kwa takribani miaka mitano hivi, lakini Bibi huyu hakuzaa, alikuwa hana kizazi, mnamo mwaka 1945 alimuoa Bi Mwanaasha binti              Mwinyihija Minjuma Kuchimba kutoka Mtoni Kijichi baada ya kumuacha          Bi  Tuhuma.Bi mwanaasha alizaliwa mwaka 1930 alipofunga ndoa alikuwa na umri wa miaka 16 tu.

Mzee Athumani alizaa watoto kumi  na mbili (12) na Bi Mwanaasha mnamo mwaka 1969 Mzee Athumani alimwacha Bi mwanaasha na akaolewa na mume mwingine ambaye alizaa naye watoto wawili (2) Bi Mwanaasha baadaye aliugua na kufariki nyumbani kwao Mtoni Kijichi. Mnamo August 1981. Aliishi na mzee Athumani kwa miaka takribani 36 (1945- 1981)

Mwaka 1971 Mzee Athumani alimuoa Bi Meje kutoka Buyuni waliishi miaka ishirini na saba (27) alifariki, Bi Meje hakuwahi kuzaa na mzee Athumani. Mwaka 2000 Mzee Athumani alimuoa Bi Nyapilimo Akaishi naye miaka mitano kisha mnamo mwaka 2005 akamuacha.  Baada ya hapo Mzee Athumani aliendelea kukaa bila ya mke hadi pale alipofariki 29/09/2008.  Bi Nyapilimo alifariki mwanzoni mwa 2012.
 Mzee Athumani hadi anafariki aliacha watoto wake walio hai wakiwa tisa ( 9) sita wanaume na watatu wanawake  Hata hivyo baada ya muda si mrefu watoto wake wawili walifariki, kwanza Bi Jamila Athumani aliyefariki tarehe07/02/2009   na baadaye Bw Talib Athumani aliyefariki tarehe 05/07/2009  miezi mitano          baadaye huko Boswana Gaberone na kuzikwa Mbagala Kizuiani maskani ya ukoo wa Seseme.   Watoto wengine wa mzee Athumani waliofariki huko nyuma ni kama ifuatavyo:
1. Hussein athumani                  amezaliwa  1948   amefariki 1949
2. Chausiku Athumani amezaliwa 1950 amefariki  1952
Hadji Athumani amezaliwa  1956 amefariki  1997

Hadi sasa watoto walio hai ni saba (7) wakiwemo wanaume watano (5) na wanawake wawili (2) Watoto hao wanaume ni Hassan, Salama (Bapoo),            Muharami, Omari na Ishaka wanawake ni Subira na Salima.

Mzee Athumani Hussein ni mmoja wapo kati ya mifano bora kwa binadamu kuiga kwani siyo siri yeye amefanya mengi mno katika uhai wake kwenye ukoo ambayo wengi wetu hatujayafikia mambo hayo. Mzee Athumani hakua mbaguzi katika ndugu zake na hata wasio kuwa ndugu zake.

Mzee Athumani tokea miaka ile ya 1950 wakati wazee wetu watatu wote wako hai akina mzee Hussein Hussein, Omari Hussein na Abdallah Hussein                       wameshampa fursa ya kuongoza ukoo.

Naye akakipokea cheo hicho kwa roho moja na kukitendea haki. Hii ni            kutokana na tabia yake ya uadilifu.Dhamira ya mzee Athumani kwa ndugu zake ilikuwa ni kuwafikisha mbali kimaisha.

Na katika kuonesha jinsi alivyodhamiria kuwapeleka mbele kimaendeleo ndugu zake hao, wengi kati yetu alitulea kwa kutusomesha na kuhakikisha tunakuwa na maisha bora hapo baadaye,licha ya kuwalea wanawe wa kuzaa mwenyewe kama ilivyo wajibu lakini pia Bwana Jaffar Hussein Seseme, Mwishehe, Ashura, Ally na Husna ni kati ya wanandugu ukoo wa Seseme aliowahi kuwalea. Bwana Azizi  Kuchimba, Bi Zena Kuchimba nao ni miongoni mwa hao aliowahi kuwalea.  Hawa wakitokea upande wa mkewe. Pamoja na hao kuna wengine wengi aliopata kuwalea waliotokea aidha upande weke ama kwa mkewe, wote hawa aliwaona ni sawa hakujua kubagua.

Watu walimsifu kwa uungwana wake wamesema kuwa Mzee Athumani                    alikuwa ni muhimili mkubwa katika ukoo wa Seseme kwani hakujua kubagua yoyote wote kwake yeye walikuwa sawasawa mbele yake. Kwa kifupi cha             maneno Mzee Athumani alifananishwa na Jemedari shupavu, Amiri, Khalifa na Imamu katika ukoo wa Seseme.

Bwana Athumani wakati wa mazishi yake pale Mbagala Kizuiani watu wengi mbalimbali walihudhuria, wakubwa kwa wadogo, wake kwa waume. Hiki                 kilikuwa kielelezo tosha cha umaarufu wake.




Jumatano, 30 Januari 2013

UTAMADUNI WA WAZARAMO


MJI WA DAR ES SALAAM.

Mji wa Dar es Salaam hapo awali ulijulikana kama MZIZIMA wala hapakupata kuwapo na habari zenye ukamilifu juu ya chanzo cha jina  hilo, bali kuna mapokeo mbalimbali yenye  kueleza tu chanzo chake.

Mathalani, yapo mapokeo yanayoelezea kuwa katika mwaka 1866 Sayid Majid (Mwarabu) Mtawala na mfanyabiashara tajiri toka Oman inasemakana  uliujenga mji wa Dar es Salaam kwa kiasi Fulani na hasa Bandari ili kumrahisishia upakuaji na upakiaji wa bidhaa zake mbalimbali ziingiazo na zitokazo kwa njia ya baharini.

Kutokana na hali nzuri sana ya utulivu na usalama wa bandari           walivyoiona wakati wakishughulikia mizigo yao, wakaamua kuita             Bandari hiyo kuwa ni ya salama.  Jina hili lilizoeleka  mno  hatimaye likawa ndio chanzo  cha mji wote kuitwa Bandari ya salama na           baadae ikawa Dar es Salaam kama ijulikanavyo hadi hivi sasa.

Mapokeo mengine juu ya jina Dar es Salaam ni kwamba, inasemakana kuwa walikuja Mzizima wahindi wawili wafanya biashara enzi hizo mmoja  akiitwa Butu na mwingine Salama.  Wahindi hao   walijenga nyumba mbili kubwa, kila mmoja na yake.  Nyumba hizo za biashara  ziliitwa mabanda.  Wakulima kutoka shamba walikuja Mzizima kuuza na kununua bidhaa mbalimbali kwa wahindi hao. 

Katika hali isiyoeleweka wakulima hao walivutiwa mno kufanya              biashara ya kuuza ama kununua kwenye banda la Salama kuliko             Banda la Butu.

Hivyo basi wakulima hao walipokuwa  wakikutana njiani walipoulizana kama walinunua ama kuuza wapi bidhaa zao, jibu mara nyingi             lilikua Banda la Salama  ama kama ilivyozoeleka hivi sasa                    Dar es Salaam.  Kuna  mapokeo mengine juu ya kupatikana kwa jina la  Dar es Salaam kama ifuatavyo.

Inasemekana kuwa Wazungu walipotaka kuingia nchini Tanganyika (Tanzania) Waarabu ambao walitangulia kuja humu nchini kabla yao yalizuka mapigano makubwa kati yao hususan wajerumani na Waarabu, enzi hizo mtawala mzalendo  alikuwa Mwinyimkuu Mshindo,             mapigano hayo yalipofika mzizima ikapatikana suluhu kupitia          mazungumzo, mapigano yakaisha.  Hivyo  sehemu hii ya mzizima        ikapata   jina la Bandari ya Salama kutokana na amani iliyopatikana wakati huo.  Kwa hivyo jina la mzizima likabadilika badala yake         pakaitwa
Banda la salama
Bandari salama
Bandari ya salama
Na hatimaye pakaitwa D’Salaam, Jina litumikalo hadi hivi sasa.




Wakati huo huo Bwana Hatimi Mfanya Biashara ya Chumvi  Mwarabu alifika kwenye  mwambao huo akaleta chumvi na akaoa mjakazi, binti wa Kishirazi na akabahatika kupata mtoto mmoja wa kiume.

Kwa kuwa Bw. Hatimi ndiye aliyeleta chumvi basi mtoto huyo akaitwa chomvi (chumvi)  na baadae jina la chomvi likabadilika na kuwa shomvi, na kizazi chake kikaitwa Wamashomvi.

Inasemekana  kuwa Wamashomvi  ni mchanganyiko wa Waarabu na wenyeji  wa pwani ya Dar es Salaam.

NB:  
Kutokana  na maelezo ya Bwana B.A. Kando ya juu ya upatikanaji wa chumvi bila shaka kuna tofauti ya ugunduzi wa chumvi na uchuuzi wa chumvi kama ilivyokuwa kwa Bwana    Hatimi. Yeye hatimi alikua mchuuzi wa chumvi, lakini siye aliyegundua chumvi.

SULTAN SEYYID MAJID NA WAJERUMANI.

Sayyid majid hapo mwanzoni aliogopa sana utawala wa Pazi.               Wazalendo aliowakuta akitokea kwao Oman Uarabuni.

Kwa sababu ya kutafuta mali kwa ajili ya maisha, Sultani majid           alilazimika kuhamia Mzizima kunako Mwaka 1862 na Mwaka 1865 alianza kuujenga mji wa Dar es Salaam kwa kiasi Fulani.

Lakini, mnamo mwaka 1885 Wajerumani waliingia Mzizima na katika mwaka 1886 walianzisha utawala wao. Wajerumani   waliweza kuitawala Tanganyika walipomtumia mtu wao mjanja mjerumani Karl Peters ambae mnamo 1885 alifanikiwa kufanya mikataba ya kitapeli kwa  kuwahadaa Machifu wazalendo hapa nchini.  Chifu Mangungu ni mmojawapo  aliyetiliana mkataba  na Karl Peters.  Hatimaye kuanzisha dola yao mnamo mwaka 1885.  Katika mwaka huo huo Wajerumani waliweka   mpaka ya nchi Tanganyika ili waweze kuendesha dola yao bila hofu ya kuingiliwa na mataifa mageni mipaka hiyo  inatambulika kimataifa hadi hivi sasa.

Mwaka 1893,  Wajerumani  wakiunganisha na msaada wa mfanyabiashara Mwarabu  tajiri wa Bagamoyo Sheikh Sewa Bin Hadji walijenga Hospitali kubwa ya kulaza wagonjwa pale palipokuwa pakijulikana kama Malindi, eneo  la Bandari  ambalo karibu na kituo cha kati cha Polisi (Central Polisi Stn).  Sewa Hadji alichangia Rupees 12,400  ambazo kwa wakati huo zilikuwa pesa nyingi sana.

Mwaka 1894  Wajerumani walianza kujenga Reli ya kati (Central line).  Na katika mwaka 1914 Wajerumani walijenga soko la Kariakoo. 



Lengo na madhumuni ya ujenzi huo hasa ilikuwa kuadhimisha                  kutawazwa kwa mfalme wao Kaiser Wilhem huko Ujerumani .  Lengo  hilo hata hivyo   halikutimia, kwani mwaka huo huo  vita kuu ya            kwanza ya dunia ilianza na kuvuruga mpango mzima.


Vita hii huku kwetu ilikua kati ya Waingereza na Wajerumani  na hata  Wazalendo walihusishwa kwa namna moja ama nyingine.                           Waliposhindwa Wajerumani, Waingereza walichukua hatamu  ya           uongozi wananchi hii kunako mwaka 1921. 
Jengo hilo la soko likatumika kama kambi  ya Jeshi ya kuwekea vifaa vyao vya vita.  Kwa Kiingereza waliita  “Carrier Crops” Waswahili katika kukosea matamshi waliita” Kariakoo” Jina  maarufu ambalo linatumika hadi hivi sasa.


Kama  ilivyokuwa kwa Wajerumani, Waingereza  nao walianza  na Ujenzi wa shule ya Uhuru wavulana Mwaka 1921.  Enzi hizo ilijulikana kama Kichwele Boys  Middle School.  Na mwaka  1935 wakajenga shule ya Uhuru  Girls Middle School.  Wakati huo ilijulikana kama Kichwele Girls Middle School. Na kunako Mwaka 1939 walijenga       shule ya Mchikichini Primary  School.


Mwaka 1949 ilianzishwa Kampuni ya usafiri Dar es Salaam iliyoitwa kwa kifupi DMT ama Dar es Salaam Motor Transport.  Kampuni hiyo ilibadilishwa jina baada ya uhuru wa Tanganyika na kuwa shirika la usafiri  la Taifa na kuligawa sehemu mbili (UDA/KAMATA).


UDA – Usafi Dar es Salaam na KAMATA – Kampuni ya Mabasi             Tanzania ambapo Kampuni hiyo ya mabasi hayo yalibuniwa ili kusafiri mbali, Bara na nje ya Tanzania, kama vile Kenya Mombasa na Nairobi, Kampala Uganda, Ndola Zambia na kadhalika. Mpango huu                   ulianzishwa rasmi mnamo mwezi Julay 1969 uamuzi wa kuunda Kampuni  hizi  za  usafiri Dar es Salaam   na bara ulianza  kutokana na ongezeko  la haraka  la idadi  ya wakazi wa Dar es Salaam hasa, na ingawa nchi nzima ya Tanzania idadi ya watu ilikuwa  ikiongezeka kwa kasi kila uchao lakini toka hapo mwanzo ilionekana kuwa Dar es Salaam ndio mji ambao watu wake wanaongezeka kwa kasi zaidi kuliko maeneo mengine ya nchi.



Mr. L. W. Swants, Mwandishi mmoja kati ya vile vitabu vinne                  alivyozungumzia mwandishi wa simulizi hii.  Katika kitabu  chake The Zaramo of Dar es Salaam, amesimulia jinsi ya kuongezeka  kwa wakazi wa Dar es        Salaam kuanzia Mwaka 1957.  Bw. Swants     ameainisha  kuwa pamoja na  wakazi wengine kufikia mwaka huo Wazaramo pekee walikuwa 33, 960 Dar es Salaam.  Idadi  hiyo            ilikuwa ni asilimia 18.5%  ya wakazi wote wa Dar es Salaam kwa wakati huo.  Na baada ya hesabu za sensa katika mwaka huo idadi ya wakazi wote wa Dar es Salaam walikuwa 183,260.


MUHIMBILI HOSPITAL

Itakumbukwa kuwa , hapo nyuma kidogo  kabla ya kujengwa  Hospitali ya      Rufaa ya Muhimbili.  Hospitali kubwa ambayo   ilifananishwa na Muhimbili ni Sewa Hadji Hospitali.  Hospitali hii   ilijengwa wakati  wa utawala wa Wajerumani kama tulivyokwisha eleza hapo nyuma.


Hospitali  ya Sewa Hadji ilikuwa pale Malindi karibu na Central  Polisi Station eneo ambalo hivi sasa linatumika na Bandari baada ya Jengo  hilo kubomolewa kwa upanuzi wa Bandari hiyo.


Wajerumani vile vile katika Mwaka 1897 walilifungua rasmi jengo  jingine la Hospitali  ijulikanayo hadi hivi leo The Ocean Road   European Hospital.          Hospital ambayo kwa hivi sasa inatumika maalum kwa magonjwa ya Saratani.


Waingereza walipokaribia kutoa uhuru wa Tanganyika walijitahidi katika kujenga baadhi ya majengo kama vile walivyojenga majengo ya   Hospital ya Muhimbili.  Hapo zamani Muhimbili palikuwepo na   mabanda madogo tu eneo la sasa ilipo University of Dar es Salaam     Facult of Medicine  ambayo yalikuwa yanajulikana kama Muhimbili Hospitali na matumizi yake ilikuwa utibabu hasa wa kina mama  wazazi wajawazito  na huduma nyinginezo ndogondogo. 

Hapakuwa pakilazwa wagonjwa kama hivi  sasa.  Waingereza kwa                hivyo wakajenga Hospital kubwa ya kulaza wagonjwa walipomaliza  kuijenga Hospital hiyo kwa fedha zao Princess Magret mdogo wa Malkia Elizabeth II alikuja kufungua rasmi  mnamo Mwaka 1957  alipokuwa ziarani Tanganyika.  Jengo hilo  likaitwa Princes    Margreth   Hospitali kwa heshima yake.  Princess Magreth ameshafariki hivi sasa.

Jina  la Sewa Hadji lilipendekezwa kuwepo pale Muhimbili kwa               madhumuni ya kumuenzi mfadhili huyo.Kwani ilipobomolewa                    Hospitali ya Sewa Hajji kule karibu na kituo cha kati cha Polisi, enzi zile  palijulikana  kama Malindi hapakuwahi kuwepo jina la Sewa Hadji popote  Tanganyika bila shaka wakubwa waliona haingekuwa ni    uungwana kumsahau mtu  aliyejitolea kuwahami  wananchi wengi wa    Tanganyika siku hizo bila ya kuwepo kumbukumbu yake ndipo jina lake likaingizwa katika mashujaa wetu.   Na bila shaka Mashujaa wetu wazalendo  Kibasila na Mwaisela habari zao zinaeleweka vyema katika Historia ya nchi yetu ya Tanzania.



UTAMADUNI WA WAZARAMO (LUGHA)

Bila shaka kila kabila duniani lina utamaduni wake na lugha yao ya asili ya mawasiliano. Wazaramo halikadhalika wanautamaduni wao na lugha yao ya asili ya mawasiliano.  Lugha yao ya kizaramo ni maarufu na ni moja kati ya lugha za zamani sana katika jamii ya Watanzania .  Wazaramo  baadhi yao hasa wazee  wale wa vijijini ni mahiri sana wa kuongea lugha yao hadi hivi sasa  kinyume na wale wazaramo waishio mijini hususani Dar es Salaam.  Wengi wao hawawezi kuongea lugha hiyo kwa ufasaha, napengine si ajabu  kutoifahamu kabisa.  Athari ambayo huenda imeanzia toka kuzaliwa kwao.  Hii imetokana na wazee wenyewe kutowafundisha vizazi vyao, tokea udogoni.  Kutokana  na taathira hiyo  basi lugha ya kizaramo  imekuwa ikipoteza umaarufu wake kadri ya miaka  inavyosonga mbele.

Lawama , hii kwa hivyo moja kwa moja inabebwa na wazee wenyewe kwa kutokuwa makini kwa kutoitilia lugha yao mkazo toka zamani katika  kuiongea mara kwa mara ili na vijana wao wapate  kuiga, kwa hivyo basi polepole lugha hiyo ikaanza kusahaulika hususan kwa wale waishio mijini hasa na hivyo basi hatimaye hata huko vijijini pia.

Pamoja na kwamba bado kuna baadhi ya Wazaramo ambao wanaongea lugha yao hiyo lakini hawaongei kwa ufasaha na wala si wazungumzaji wanaoipa umuhimu wa kutosha.


Kwa kuwa si Wazaramo wengi wanaoiongea  lugha hii hivi sasa hata huko vijijini dalili za kutoweka kabisa ni dhahiri katika muda si mrefu  sana ujao, iwapo kama hatua za  dhati kuinusuru hazitachukuliwa haraka.

Kumbukumbu zetu zinaonesha kuwa lugha ya Kizaramo katika ukoo wetu wa Seseme, imeachwa kabisa kuzungumzwa toka wakati ule wa Mababu na Mabibi zetu kina mzee Hussein Hussein Seseme                       takriban sasa miaka mia na hamsini iliyopita hivi. Mzee Hussein na nduguze wawili mzee Omar na Mzee Abdalah hawakuwa na mazoea  ya kuzungumza lugha ya kizaramo waziwazi badala yake waliipa kipa       umbele lugha  ya Kiswahili, lugha ambayo wameichukulia kama  lugha yao mama.  Hapakuwepo na mkazo kabisa katika   kuzungumza kizaramo matokeo yake vizazi vyote katika ukoo huu wa Seseme hatuna taalum ya lugha hii.

Lakini janga hili la kutokomea kwa lugha ya kizaramo                         halikuanzishwa na ukoo wa Seseme tu bali ni kosa lililotendeka na jamii



NGOMA ZA HARUSI NA SHEREHE ZINGINEZO.

Inasemekana kuwa Wazaramo walikuwa na mkusanyiko mkubwa mno wa ngoma za asili  hata yawezekana kuwa ni moja kati ya               makabila yenye ngoma nyingi mno katika Tanzania ingawa nyingi sasa zimeanza kutoweka.  Ngoma hizo hasa huchezwa nyakati za sherehe mbalimbali kama  vile kwenye harusi unyago, mkole kwa mabinti wanawari, suna ama jando kwa wavulana ambapo mangariba hucheza ngoma ya msewe na sherehe zingine kadhalika katika kutekeleza kazi yao.
                                                                                                   
Ngoma za Wazaramo baadhi y ake zina mgawanyiko wa tofauti ya watu umri na jinsia.  Vijana wadogo huwa na aina yao ya ngoma, watu wa makamo pia huwa na namna yao.  Hali kadhalika wazee wake kwa waume  kila mmoja huchezwa kivyake.  Lakini kuna vile vile ngoma za mjumwiko wa jinsia zote na umri wowote, hizo  ndizo nyingi mno na ndio hizo furaha za Wazaramo na ngoma zao hizo za asili Ngoma mathalani mkole na msondo  ni  ngoma zinazowahusu kina mama  na kina dada vijana na kadhalika.

Ngoma hizo kwa kuzitaja majina yake ambazo nyingi mno ni,               Mdundiko,  Msondo, Vanga ama Mkinda, Mkwaju Ngoma, Matarumbeta ama Beni bati Mnanda ama Mchiriku, Mganda, Buti na kadhalika.

Na hapo  siku za nyuma kidogo palikuwepo na ngoma ambazo hivi sasa husikika kwa nadra sana ama  hazipo tena, kutokana na kupoteza kabisa umaarufu wake, ngoma ya Tokomile kwa mfano ilipoteza umaarufu wake kutokana na kufutwa kwa uhasama wa kijadi wa ngoma hiyo ambapo Mbango na Mizia  mahasimu  wakubwa walisababisha  mapigano  yasiyo na faida yoyote zaidi ya kumwaga damu bure tu kwa wananchi ambapo kinyume chake walikuwa wajenge umoja ili kuundoa ukoloni wa Mwingereza enzi zile kabla ya uhuru badala ya kuwa mbwa na chatu .

Mwalimu Nyerere  wakati ule akiwa Mwenyekiti wa TANU chama  kilichodai Uhuru wa nchi hii Tanganyika, rai yake kwa wananchi kuwa ngoma hiyo ichezwa bila ya silaha ili kuepusha  mapigano  na kumwaga damu kwa kuwataka Mbago na Mizia mahasimu hao wa jadi wapatane ili wawe kitu kimoja jambo ambalo  lilionekana kama gumu sana hapo mwanzo lakini  iliwezekana baadae  uhasama ukamalizika   na hatimaye ngoma yenyewe kufa kabisa.   Siku hizi si rahisi kuisikia ngoma ya Takomile. 



Kwa hakika ngoma ya Tokomile haikuwa ngoma ya amani, kama ilivyo desturi ya ngoma nyingi, kwani watu badala   ya kufurahi  walifanyiana uadui, ingawa Wazaramo wenyewe waliita ngoma ya mashujaa,   hasa kutokana na yale mapigano baina ya pande mbili  Mbango na Mizia lakini sababu hii haikuwa ya msingi hata kidogo. 
Visa vingi viliwahi kutokea enzi hizo  vya umwagaji wa damu na mara nyingine hata kusababisha  vifo, kwa hivyo badala ya furaha ikawa ni misiba na vilio, jambo ambalo halikuwa na maana yoyote.

Ngoma ya Tokomile kwa makusudi kabisa wahusika walianzisha vurumai  wakapigana ati kuonesha nani mbabe zaidi kati yao, hilo tu basi.  Wala hapakuwepo na lolote la maana. Mwisho wa yote wakajikuta katika   hasara  kubwa.  Ngoma zingine zilikufa kifo cha kawaida.  Ngoma  kama vile Ndalandala Mtondoo Lelemama Kasangwa, Ndekule.  Sikinde na kadhalika.  Ngoma hizo zilipata kuchezwa zama hizo za wazee wetu, Mababu na Mabibi, Vijana wa kizazi cha sasa si wengi walioweza kubahatika kuzishuhudia ngoma hizo zikirindima.  Hivi sasa ngoma hizi imebakia hadithi tu kusimuliwa  hamna la zaidi.
Kuna baadhi ya wanamuziki wa sasa wameziingiza baadhi ya ngoma hizo katika Bendi zao za dansi kama mtindo wao, kwa maana ya ubunifu katika kuboresha miziki yao .

Ngoma ya kina mama ya msondo kwa mfano.  OTTU JAZZ imeungiza kama mtindo wao.  Sikinde imeingizwa katika Band ya Mlimani Park na hata Ndekule iliwahi kuingizwa kwenye Safari Sound Band ya Huggo Kissima Mfanya biashara maarufu Dar es Salaam  Band hiyo hivi sasa haipo tena.  Hata  hivyo  uasilishaji huu wa mitindo ya  ngoma hizo za Wazaramo katika miziki  ya dansi hazikuweza   kuzirudisha tena ulingoni  bali ni kumbukumbu tu iliyobaki ngoma hizo kuwa zilikuwepo.  Kulikuwepo pia  vanga vanga Band  ya Polisi Jazz zote  hizo ni Ngoma za Kizaramo, ambazo Band za Music zilizitumia kama kitambulisho chao





NGOMA ZA MASHETANI NA TAMBIKO.

Ukiachana na ngoma za sherehe mbalimbali ambazo kwa kawaida ni za furaha, kuna ngoma zingine ni maalum kwa uganga.  Ngoma hizo wateja hupunga mashetani, ni ngoma za tiba kwa wenye kupagawa na Pepo wabaya ama hupata maradhi yanayohusisha   mashetani   ambao inaaminika kuwa pepo hao huleta madhara kwa  watu, kuumwa hata pengine kufa kama ukipambana na madudu hayo.  Sasa , ili kumponya  muathirika basi hupungwa mashetani kwa ngoma ya madogoli, pepo hao maarufu sana ni kinyamkera na mwanambago inaaminika kuwa ni lazima watolewe kutoka mwili wa mteja.   Mteja ni Yule aliyepatwa na mashetani hao, hivyo mganga wa mashetani hulazimika kupigisha ngoma ya madogoli ili kumnusuru mgonjwa wake (Mteja)

Kwa upande  mwingine kuna tambiko za jadi.  Kwa kizazi hiki cha sasa, si rahisi sana kuelewa ama hata kukubaliana na mawazo ya wazee wa zamani hususani juu ya tambiko za jadi.  Wazee wa zamani walisisitiza  mno juu ya kufanya tambiko hizo za mizimu ya wahenga ambayo wanasema isipokumbukwa basi huenda ikaleta madhara makubwa kwenye ukoo mzima kama vile maradhi na hata vifo.  Tambiko  huwa kinga kwa husuda na kadhalika. Wazee waliamini hivyo.


Katika ukoo wa Seseme  kwa mfano kuna tambiko la jadi linajulikana kwa jina la “GOMBO”  Bado  kuna kumbukumbu ya mzee mmoja mganga mahiri  sana katika tambiko  hii.

Akijulikana katika ukoo  maarufu kwa jina la mzee “MCHAFU” Hata  hivyo walikuwepo  akina mzee Mchafu wengine  wengi walioifahamu  vyema “GOMBO”  ala za ngoma hii ya Tambiko ni ungo wa kupetea nafaka,  pamoja na udananda aina ya upinde mdogo ambao huwambwa kwenye ungo huo.  na kisha mzee  Mchafu ama mganga mwingine  huvuta kamba ya upinde huo  kama ilivyo namna ya udananda wa  mwari wa kike afanyavyo ama mtu apigae gitaa   upinde huo hutoa sauti ya kama mnyama Fulani aliyae kwa sauti ya  chini  chini ama sauti hiyo  inaweza kufananishwa  na gitaa la besi la Band hizi za sasa, lakini Gombo hutoa mlio mdogo zaidi wa chini   chini. 

Kwa hivyo washiriki wanaukoo  wote hujumuika katika kucheza  kwa kuzunguka zunguka wale wapigaji  wa hiyo ngoma na kuimba kwa sauti kufuatisha maneno ya mganga aimbavyo.




Aghalabu nyimbo zenyewe hazipendezi  masikioni mwa watu Tambiko  hili huanza usiku kwani huwa za matusi makubwa bila kujali mjumuiko wenyewe umehusisha watu mnaostahiyana kiuzawa, kinachozingatiwa tu kwenye mkusanyiko huo ambao huwepo Baba, Mama, Babu, Bibi, Mjomba, Shangazi, Watoto, Wajukuu vilembwe na kadhalika ni ile miiko yao inayoruhusu kufanya hivyo ilimradi uganga utimie tu, wanavyoamini,  hakuna tusi lolote litamkwalo litakalochukuliwa kama ni uvunjifu wa adabu, lau kama mtu atatukuna mbele ya mamaye ama babayake mzazi ama mzee yoyote ilimradi tu yupo katika  tambiko  hiyo basi yeye ni ruksa tu.  Na hiyo ndiyo hasa maana ya “GOMBO”

Kwa hakika nachelea mno iwapo kamaTambiko  la sampuli hii linawezekana kufanyika tena kwa uwepesi sana katika nyakati zetu hizi zenye nidhamu bora ya kidini, hususani dini yetu hii ya Kiislam, kama ilivyokuwa hapo zamani.

Kwa mujibu  wa mafunzo  ya dini ya Kiislamu  ni kwamba  Uislam haushirikishwi  kwa vyovyote vile na mashetani, kwani mambo ya kishetani tayari yamelaaniwa kwenye Quraan Tukufu hivyo basi hayakubaliki Abadan.



Kwa  asilimia kubwa sana Gombo linahusisha ushetani na si ajabu hata ushirikina  pia umo.  Hivyo tahadhari  inalazimika sana.

Nyimbo ziimbwazo katika  Gombo ni za matusi ya nguoni, lakini  hakuna mwiko  katika kuimba matusi hayo, hata kama utaimba mbele za watu  mnaostahiliana kinasaba.

Gombolillaga x 2  kolila naumoyo Gombo kolilla naumoyo” x 2
Waganga huimbisha hivyo na wanandugu hulazimika kuitikia kwa kufuatisha maneno hayo kwa sauti kubwa ya  kuhinikiza  huku ngoma ya Gombo ikirindima.

Wengi  katika  sisi wanandugu, wajukuu wa akina mzee  Makumbitu tukiwa tumechanganyika na wazee wetu, Baba zetu mama zetu shangazi zetu na kadhalika tumekuwa  ni watu wa kufuata amri tu kutoka kwa wazee hao, lakini  hatukupewa nafasi hata chembe kuhoji jambo lolote lile juu   ya utamaduni huo wa Gombo, kwani kufanya hivyo ni kutaka kujua kile kinachoendlea katika  tambiko hilo linalochukuliwa  na wadau kama ni kuwakosea  adabu wazee.  Bila shaka jambo likishafikia hatua kama hiyo basi huwa halina sululu tena, bali ni kuacha tu amri ya wazee ichukue mkondo wake, na hivyo basi ndivyo ilivyokuwa.



Ngoma hii watu hukesha wakicheza na kuimba usiku kucha wakiwazunguuka zunguuka wale  waganga walioketi katikakati yao, mithili ya mchezo wa kitoto wa Foriti.

Hakuna  staili maalum ya uchezaji ngoma hiyo, ila wewe cheza tu vile uwezavyo na tamka matusi  uyajuayo  wala usiogope  jambo lolote kwani hakuna mtu atakayekukosoa atakayesema kuwa wewe huna nidhamu.  Kwani hivi ndivyo hasa Tambiko ya Gombo litakiwavyo.  Tusi huwa si tusi katika Gombo bali huwa kinga kubwa  dhidi ya maadui wetu kwa mujibu  wa wazee wetu walivyoamini.  Tambiko la ukoo wa Seseme”
Ifikapo  Alfajiri wakati adhana inaposikika swala ya Kiislam huwa ndio kikomo cha Tambiko.  Nyimbo za mwisho mwisho kumalizia shughuli nzima ya Tambiko, wanganga  husikika wakiimbia:
“Sanze Mnumanunma, Sanze Mnumanuma, Kupitita bahano kadimanula manu, Sanze mnumanuma x 2”

Wimbo  huo  hurudiwa tena na tena, wanandugu hufikia na hatimaye mwimbo humalizika kuashiria kwisha kwa Tambiko. 
Mganga Mkuu huamrisha wanandugu waliopo kwenye  Gombo wakusanyike chini ya mti mkubwa ambao Gombo hufanyika, na kuamuru kila mtu kumega tonge moja la ugali uliopoa, ugali wenyewe huwa  aidha wa ulezi  au mtama lakini si wa mahindi.  Pia kunyofaoa kipande cha nyama ya kuku  wa kubanika wa dawa aliyepoa na kumeza mchangayiko  bila kunywa maji wala kutafuna mfupa.
Kawaida miti iliyopendekezwa hasa kwa tambiko ni Mbuyu Mvule Mwembe na kadhalika.

Mifupa ya kuku, manyoya  na utumbo hufukiwa pale chini ya mti pamoja na chungu kile kilichopikiwa ule ugali.


 Wakati  wa kuchimbia na kufukia chungu hicho cha dawa mganga mkuu huomba kwa niaba ya wanadungu mambo ya manusura  katika Afya na kipato katika mwaka mzima husika  maombi hayo hupitishwa kwenye mti ule.

Baada  ya hapo mganga  mkuu hutoa ruhusa ya wanandugu  kurudi majumbani mwao hadi mwaka mwingine kwa ajili ya tambiko jingine.

Masharti ya Gombo ni kwamba nyimbo zile za Tambiko za Matusi ni lazima ziimbwe  tena kwa sauti kubwa ili walio mbali  waweze kusikia vyema  nini kinachoimbwa.

Tena ziimbwe nyimbo hizo bila kuona haya wala kuweka staha kwa wazee mliojumuika nao, na bila ya  kujali aina gani ya matusi yaimbwayo.

Wazee wetu waliamini ya kuwa gombo ni lazima katika ukoo huu wa Seseme, pamoja na kwamba hapakuwepo na maelezo yoyote ya kisayansi waliyoyaacha wazee  hao juu ya umuhimu na ukweli  hasa wa jambo hilo wanaloliamini kupita kiasi.

Jambo la ajabu kuhusu wazee  wetu ni kwamba pamoja na wao huwa waumini wa dini ya Kiislam, dini ambayo inakemea vikali sana ushetani, lakini wao waling’ang’ania  utamaduni wao huo walioachiwa na wazee wao, wa Tambiko la Gombo.  Waliamini kuwa Gombo ni kinga kubwa sana katika ukoo.

Jambo  hili kwa sasa linamvutano  mkubwa sana baina  ya Wazee na vijana, kuhusiana na Tambiko hilo la Gombo.

Sikuhizi Gombo hutekelezwa kwa shinikizo la wale wenye umri mkubwa kwa kuwapa maelekezo wadogo kama amri tu.

Lakini hapana shaka kuwa wakubwa hao katika ukoo nao ni waathirika wa mawazo ya wazee wao, Babu zetu.  Kwa mantiki hii bila shaka Gombo sasa linaelekea kwenye hatima yake.



MARUHANI

Maruhani  ni aina nyingine mojawapo ya mashetani, lakini husemekana kuwa ni mashetani wema kwa Binadamu. Kwani hufanya kazi ya tiba za maradhi mbalimbali badala ya kuwadhuru.

Wazee  waliyatilia maanani  sana Maruhani . Inasemekana kwamba yanaweza hata kuagua uchawi  kwa mtu aliyerogwa.

Kwa  kawaida  huwepo waganga wanaotumia hawa maruhani katika  ukoo.

Kwamba  mtu  aliyerogwa, shetani wa maruhani huwa na uwezo wa kugundua maradhi na mchawi aliyemroga  mtu huyo.

Hivyo  basi mganga wa maruahani huitwa kuja kumuagua mteja aliyerogwa  .

Maruhani kwa jumla huwepo takribani  katika  kila ukoo hususan enzi hizo.  Madhumuni hasa ya kuwepo hao maruhani ni kutibu inapotokea mtu kurogwa na kadhalika.

Hata  hivyo kwa kusema hivyo sina maana ya kuwa Wazaramo walipendelea  majini na uchawi la hasha bali hii ni kujulisha tu kwamba Wazaramo kama walivyo binadamu wengine wanafikwa na mambo mengi ya  kidunia kama ilivyo kwa watu wengine  wote hapa ulimwenguni.


UTANI  KATIKA UZARAMO.

Kuna  baadhi ya watu walikuwa wanawachanganya Wasukuma kama vile Wanyamwezi kwamba  na wao pia ni watani wa wazaramo lakini kwa uhakika  Wasukuma si watani wa Wazaramo ila tu kwa vile wasukuma na Wanyamwezi wanafanana  mno  katika mambo yao mengi hivyo basi moja kwa moja nao wamekuwa watani wa wazaramo.

Katika kutafiti ili kujua utani huo wa makabila haya ulianza vipi kwa  kweli  jibu lake halikupatikana bila shaka wazee wa zamani wanaweza kupata ukweli ulivyokuwa.  Vile vile  ndani ya Wazaramo wamo watani wanaotaniana wenyewe  kwa wenyewe kwa mfano wanzala ni watani wa wavilindi na kadhalika.

Kuna utani pia kati ya Babu ama bibi  na wajukuu  zao.  Utani kati ya mtoto wa mjomba na shangazi.  Muhile kwa muhile na kadhalika.

Kwa mfano kuna utani wa mjukuu wa kiume na Babu na Bibi yake  ulioandikwa na mtunzi mmoja BW. M. R. KIZARA katika kitabu chake UTANI wa TANZANIA (1975) Tunanukuu.

Mjukuu -  Babu lelo nokwiza ikilo kuwasa na mtwanzi wako,
                   minyusile vinhugwe kwisha tena - “Zua diswa”
Babu:  -    Ikimbigalo kunacho mina cha kuwasa na
                   mtwanzi wangu.


Mjukuu: -   Nielekelelo ulole
Babu:      Segela hano govijo
Mjukuu: -   Mbona koninga kodomba choni, nielekele ulole
Bibi: -    Ikimbigalo kunacho avo cha kuwasa na nie?
Mjukuu: -    Kama na bule mbona babu koninga kodumba msiwase
                    nangwe, leka aniluhusu ulole

Japo kuwa utani huu, unahisia kali sana,  za ndani kihalisia, bado ulikua  unakubalika katika jamii ya Kizaramo pasipo lawama zozote. Sina hakika sana kama hadi sasa utani kama huo unawezekana ukavumilika hata hivyo. 

Bwana KIZARA  ambaye  amewahi kutembelea sehemu  nyingi  waanakoishi Wazaramo kama vile  Msanga, Sungwi,  Masaki na kadhalika, ametubainishia kuwa Wazaramo hawana watani wengi kama ilivyokuwa baadhi ya makabila mengine Tanzania



Bwana Kizara ameongeza kusema kuwa Wazaramo ni kabila tulivu mno ambalo halikupenda mapigano na jirani zao katika zama hizo na  hata  hivi sasa.

Ndugu  wa Wazaramo hasa toka hapo asili ni Wakutu, Wadoe, Waluguru, Wakwele kwa vile wote hawa wanatokana na ukoo wa Pazi Kilama Lukali.  Wazaramo toka enzi hizo walikuwa ni watu  wapendao ushirikiano, urafiki, utani hasa kwa watani wao.  Kwa jumla ni watu waliopendelea sana amani, hawakuwa wachokozi kwa hivyo hawakupenda kabisa vita kama ilivyo kwa baadhi ya makabila mengine Tanzania.

POSA ZA JADI ZA WAZARAMO.

Kwa kuwa tumepitia katika maeneo mengi mno kuhusu maisha ya Wazaramo na Tamaduni zao tumeona ni vyema pia tukaingiza jambo hili muhimu sana katika maisha  ya binadamu duniani, jambo lenyewe si jingine bali ni “ndoa”.

Katika siku za nyuma kidogo mnamo   Mwaka 1920 na kurudi nyuma masharti ya ndoa ya Kizaramo yafuatayo hapa chini  ilikuwa ni lazima  yafuaatwe iwapo wanandoa wawili inapofikia wakati wa kuhalalishwa kuoana vinginevyo ni vigumu  mume kupata mke kwa namna yoyote ile, mambo yenyewe ni :-

Mahari
Mkaja
Kilemba
Behobeho

Kanyaga lubuga
Kisamula ndevu
Kilomo kinona
Mama Ngwaya
Kakulongela nani hano kama kuna Mtwanzi na kadhalika.

Baada  ya Msululu  wote huo kutimizwa ambayo tafsiri yake ni pesa ndipo ridhaa ya wazee kutolewa kwa binti yao kuolewa na               muhusika.

Katika maandalizi muhimu ya harusi kuna ngoma mbalimbali  ikiwemo mkole pia mwari kualikwa kuchezwa  na kadhalika.  Hapo mwari hufunzwa mengi kabla ya kuolewa  lakini kama tulivyosema kuwa mambo hayo ni ya asili  na yalitumika enzi hizo, lakini  mengi kati ya hayo  hivi sasa hayapo tena, na wala kizazi cha sasa hakina habari kabisa na utamaduni huu na kama yapo  basi ni kitchenparty  ambapo ni utamaduni wa kizungu hivyo mkole kwa sasa haumo katika mfumo wake wa zamani kwani  mambo yameshageuka kabisa, badala  yake ndio hiyo kitchen Party.